Friday, July 9, 2010

KUANZISHWA KWA RANCHI, NA KUTENGWA KWA MAENEO MAALUM KWA AJILI YA MALISHO YA MIFUGO NA KUNENEPESHA NA HATMA YA WAFUGAJI ASILIA TANZANIA

KUANZISHWA KWA RANCHI, NA KUTENGWA KWA MAENEO MAALUM KWA AJILI YA MALISHO YA MIFUGO NA KUNENEPESHA NA HATMA YA WAFUGAJI ASILIA TANZANIA.(By Valentin Ngorisa Olyang iri.......a paper presented to TBC One Radio)

Utangulizi

Kwa muda wa miongo miwili sasa kumekuwa na majadiliano na utungaji wa sheria na sera mbalimbali zikiwemo za Ardhi, wanyamapori, madini n.k lengo kuu ni kutatua migogoro isiyoisha na kuboresha maisha ya wananchi na taifa kwa ujumla, lakini pia uanzishwaji wa Hifadhi za Taifa, uchimbaji wa madini na maeneo mengine kwa ajili wawekezeji imepelekea wazalishaji wadowadogo ambao kwa sehemu kubwa ni wazawa kudhulumiwa ardhi zao na rasilimali zao za asili hivyo kupelekea kujiona kama watumwa na wakimbizi ndani ya nchi yao.

Moja ya namna ya serikali kutatua migogoro ya ardhi baina ya watumiaji ni kuanzishwa kwa nyanda za malisho na kufufua ranchi zilizokuwa za taifa kwa kuipa kipaumbele ufugaji wa kisasa zaidi ya ule wa asili. Kuna miswada miwili inayotegemewa kuwasilishwa katika kipindi kijacho cha bunge cha mwezi wa tano 2010.[i]

Ufugaji asili (Pastoralist) ni kitendo cha kutunza, kutumia na kumiliki mifugo kwa lengo la kujipatia mahitaji ya msingi kwa kuwafuga wanyama wa nyumbani kama ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe, punda, ngamia nk.

Kuna sababu kuu mbili zinazotofautisha aina za ufugaji

A. Kiwango cha uhamisho unaotumika (the degree of mobility practiced)

B. Kiasi cha ukaribu na wakulima (the degree of interaction with crop cultivators).

Ø Ufugaji wa kuhamahama-hawa wanahama na familia zao kwa lengo la kufuata malisho ya mifugo yao kwa muda (migrate opportunistically), pia hakuna makazi ya kudumu.

Ø Ufugaji wa transhumant- uhamaji unakikomo kwa sehemu moja husika kwa kipindi Fulani cha mwaka na kuhamisha mifugo unachukuwa tu sehemu Fulani ya familia.

Ø Ufugaji-kilimo – ufugaji unaoambatana na kilimo cha mazao ya chakula kulingana na upatikanaji wa malisho.[ii]

Katika nchi yetu ufugaji umegawanyika katika sehemu kuu mbili

§ Asili (98%)

§ Kisasa (2%)

Ufugaji wa asili unategemeana kwa sehemu kubwa na mila na desturi za kabila Fulani hivyo upatikanaji,umiliki na utumiaji wa rasilimali asilia katika sehemu husika huendana na desturi za watu.

Ufugaji wa Ranchi

Ranchi ni eneo lilotengwa kwa madhumuni ya kufuga mifugo kwa lengo Fulani na linakuwa na mipaka na kwa wakati mwingine kuwa na uzio, uliowekewa miundo mbinu ya uzalishaji. Ufugaji wa ranchi huendana na uwezo wa malisho na kufuata kanuni za ufugaji bora.

Kuanzishwa kwa ranchi Tanzania lengo kuu ni kuongeza uzalishaji na tija katika sekta ya mfugo.

Ranchi Tanzania zilianzishwa kabla ya miaka ya 1970 ambazo zilikuwa ranchi za jumuia kama Embaruai, Olmoti, Ardai n.k. Miaka ya 1970 ranchi za halmashauri kama RAZABA, MODECO,KISASIGA na USANGU. Miaka ya 1974 Ranchi za ujamaa-MWAMALASA na baadaye NARCO.[iii]

Uanzishwaji wa Ranchi unatambuliwa na Sera ya Taifa ya Mifugo ya mwaka 2006 ili kuwa na ufugaji endelevu, wenye nia ya kuinua kipato cha taifa.[iv]

Uhusiano uliopo kati ya ufugaji wa Ranchi na ufugaji wa asili

Ufugaji wa asili

Ufugaji wa kisasa (Ranchi)

Unatumia njia za asili katika ufugaji

Unafuata njia za kisasa

Ufugaji wa wazi

Ni mfumo rasmi

Umiliki wa ardhi ni wapamoja

Umiliki wa ardhi au malisho ni ya mtu mmoja au kikundi

Utumiaji wa rasilimali asilia

Unatumia za aina zote kutegemeana na wakati

Hauna gharama sana

Gharama ni kubwa (services)





Hatma ya ufugaji wa asili katika uanzishwaji wa ranchi

Kabla na baada miaka ya 1970 ranchi zilianzishwa nchini Tanzania japo ranchi hizo hazikuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo,rushwa kwenye ranchi, utumiaji mbove wa mifugo za ranch, ubovu wa miundombinu na ukosefu wa wataalam wa kutosha wa mifugo n.k.

Kwa sasa sera ya taifa ya mifugo ya mwaka 2006 inaitumbua tena ufugaji wa Ranchi kama njia nzuri ya kuongeza tija katika pato la taifa na njia endelevu kwa ufugaji wa mifugo.

Uanzishaji wa ranchi kwa nchi nzima unawezakupelekea wafugaji wa asili kuwa njia panda kutokana na sababu zifuatazo.

ü Gharama ya ranchi ni kubwa ikilinganishwa na pato la sasa la jamii ya wafugaji

ü Mifumo ya asili ya kimila itapoteza uhalisia wake na hivyo kuhatarisha mifumo ya maisha ya kimila inayoendana na mazingira.

ü Rasilimali za jamii nzima zinaweza kuwa chini ya mtu moja au kikundi cha watu fulani

ü Miundombinu za ufugaji wa Ranchi bado ni changamoto hivyo bado si njia mbadala kwa wafugaji.

ü Njia za kupunguza umasikini za kimila zitapotea na hivyo kuhatarisha ongezeko la umaskini zaidi.

ü Mbinu na namna ya kuwawezesha wafugaji bado haijawekwa sawa kulingana na mahitaji yenyewe za kibenki

Nini kifanyike (Mapendekezo)

v Kwanza, njia za asili za ufugaji ziboreshwe kulingana na mahitaji ya wananchi wenyewe.

v Pili, wafugaji wawezeshwe kwanjia zote kama kisiasa,kijamii, na kiuchumi.

v Tatu, upatikanaji wa masoko, maji, na malisho bora vizingatiwe kwanza ndani ya ufugaji wa kimila.

v Sheria zinazotungwa ziangalie uhitaji wa wananchi na si kundi Fulani la watu e.g Msawada wa utambulisho wa mifugo na mazao ya mifugo, na mswada wa ardhi ya malisho na ulishaji wa wanyama, miswada hii inategemewa kupelekwa bungeni kwenye kikao kijacho cha bunge sasa ni wafugaji wangapi wanaelewa kuhusu mswada huu?

v Tafiti zifanyike na wataalum mbalimbali juu ya faida za ufugaji wa asili na matokeo kurudishwa kwa wahusika na kukimbilia mbinu ambazo zimefeli mwanzoni.

v Elimu ya kutosha itolewe kwa jamii husika juu ya mipango ya serikali.

v Sheria kama ya Wanyapori ya 2009 kuhusu utozaji wa faini pale mifugo inapoingia katika hifadhi iangaliwe pia kwani malisho ya asili kwa wafugaji humalizwa na wanyamapori.

v Umoja wa kitaifa wa wakulima na wafugaji uundwe kuzingatia taratibu za kimila.

Hitimisho.

Ni muhimu sana kuwa na sheria ya mifugo ya jumla inayotokana na mahitaji ya wafugaji wenyewe wa ndani na si kutokana na mahitaji ya wawekezaji na pia ufugaji liwe swala la kikatiba na hivyo wafugaji kutambuliwa kikatiba kama njia ya uzalishaji mali.



[i] Daily News 31st March 2010. The Government has issued two Bills aimed at reducing land disputes between herdsmen and farmers and cattle rustling.

[ii] Muhereza, F.E (2008) Over view on Cattle rustling in the Great Horn of Africa:Knowledge Gaps and Research Interventions on Livestock Theft programme/ISS/Stakeholders meeting 14-15 May 2008

[iii] Grace Mwaigomole (2010) Kuanzishwa kwa Ranchi na ufumbuzi wa migogoro ya ardhi baina ya wafugaji na wakulima. Mada iliyojadiliwa katika semina ya HAKIARDHI 26th March 2010(LARRRI conference room)

[iv] URT (2006) National Livestock Policy: Ministry of Livestock Development.